Enos Lufungulo | Juni 10, 2020
News Brief
Bi Kimaro anaishi wilayani Moshi, katika mkoa wa Kilimanjaro kaskazini mwa Tanzania. Yeye ni mchuuzi na hupata mapato hasa kwa kuuza mazao kwenye soko. Lakini imebidi abadilishe biashara yake tangu virusi vya corona vivuruge masoko. Watu wanaogopa kuambukizwa ikiwa watatembelea sokoni. Kwa hivyo sasa, yeye hutegemea mandazi na vitumbua kwa ajili ya kupata kipato.
Kunanyesha jioni hii, lakini Sophia Kimaro yuko bize katika nyumba yake kuandaa unga wa ngano na mchele kwa ajili ya mandazi ya kesho asubuhi (madonati ya Kiafrika) na vitumbua. Yeye anasema: “Ninaamka mida ya saa kumi na moja alfajiri ili kutengeneza vitafunwa hivi. Kuanzia saa moja hadi mbili asubuhi, ninauza kwa wateja kwa kutuma [vitafunio] kwenye nyumba zao. Watu wachache huja kununua nyumbani kwangu wakati familia zingine zinatoa oda zao kwa simu. “
Bi Kimaro anaishi wilayani Moshi, katika mkoa wa Kilimanjaro kaskazini mwa Tanzania. Yeye ni mchuuzi na hupata mapato hasa kwa kuuza mazao kwenye soko. Lakini imebidi abadilishe biashara yake tangu virusi vya corona vivuruge masoko. Watu wanaogopa kuambukizwa ikiwa watatembelea sokoni. Kwa hivyo sasa, yeye hutegemea mandazi na vitumbua kwa ajili ya kupata kipato.
Anaelezea: “Badala ya kuendelea kutegemea kuuza mboga, ndizi, maparachichi, machungwa, na viazi, ambavyo wateja wanataka kwenye soko, nimeamua kubadilisha biashara. Bidhaa hizo za kilimo zinapatikana katika nyumba nyingi katika eneo langu, lakini karibu kila familia hapa inahitaji maandazi na vitumbua kwa ajili ya kifungua kinywa. “
Anaongeza, “Hata kwa biashara yangu mpya, siendi sokoni kufanya biashara kutokana na COVID-19. Ninatumia eneo la nyumba yangu kuuza mandazi na vitumbua. “
Mabadiliko haya yamepunguza sana kipato cha Bi Kimaro. Anaelezea: “Katika soko, nilikuwa napata kati ya shilingi 100,000 hadi 130,000 za Tanzania sawa na ($ 43- $ 56 US) kama faida, lakini sasa ninapata faida ya shilingi 40,000 hadi 60,000 za Tanzania, sawa na ($ 17- $ 26 US) kwa mwezi.”
Grace John anauza nyama, samaki, vifaranga, mayai, na bidhaa zingine za wanyama katika eneo lake la kuhifadhia dawa katika jiji la Arusha. Lakini COVID-19 haijaiacha salama biashara yake. Anasema, “Biashara yangu imeanguka kwa sababu ya athari za COVID-19. Idadi ya wateja imepungua kwa sababu wanaogopa kuambukizwa. “
Anaongeza: “Bado ninafanya biashara, lakini kwa njia tofauti. Badala ya kuuza kwenye bucha langu, sasa ninafanyia nyumbani. Wateja wanapiga simu au kutuma ujumbe kupitia simu ya mkononi na kutoa oda zao. Baadaye mimi hutuma kifurushi cha oda iliyotolewa kwa kutumia usafiri wa pikipiki. “
Bi. John anasema kuwa kufanya biashara kwa njia ya kutoa huduma mlango kwa mlango ni changamoto sana, na imechangia kupoteza kipato. Anaelezea: “Huu ni mfumo mpya wa kuuza na haujulikani sana kwa watu wengi. Kama matokeo, idadi ya wateja imepungua kwa sababu sio wateja wote wanaoweza kumudu gharama ya huduma hiyo.”
Jane Ngasa ni muuzaji anayeishi katika kijiji cha Nsemlwa, wilayani Mpanda Tanzania. COVID-19 pia imeathiri biashara yake. Anasema, “Hakuna soko la kuuza bidhaa na wala wateja wa kutosha kununua bidhaa.”
Bi Ngasa anasema alizoea kusambaza vyakula kama mahindi, maharagwe, na mpunga kwa wauzaji wa rejareja, na pia husafirisha bidhaa hizo kwa sehemu zingine za Tanzania. Lakini hii yote imekoma kwa sababu ya COVID-19.
Anasema, “sasa sisafirishi kwenda mikoa mingine kwa sababu biashara ya wateja wangu katika maeneo hayo imeanguka pia. Hawako tayari kuanza kununua bidhaa kutoka kwangu.
Bi Ngasa anaongeza: “Ninauza tu kwa wateja ambao huja nyumbani kwangu kununua. Hali ni mbaya na sijui ni lini itaisha. Nilikuwa nikipata faida ya hadi shilingi 350,000 za Tanzania ($ 150 US) kwa mwezi, lakini sasa ninaweza tu kupata shilingi 70,000 za Tanzania, sawa na ($ 30 US).”
COVID-19 haijabadilika tu jinsi wachuuzi wanavyofanya biashara, pia imebadilisha mitindo yao. Bibi Ngasa anasema, “Sasa hivi silipii kinga’muzi cha televisheni kama zamani. Nimeacha kununua nguo mpya kwa ajili ya familia yangu.
Licha ya ukweli kwamba COVID-19 imewataka wachuuzi wengi kuchukua mtindo mpya wa maisha, Bi Kimaro anasema ataendelea kufanya kazi kwa bidii kufanya biashara na kupata pesa kwa ajili ya familia yake, wakati pia akichukua hatua za kujilinda. Anasema, “Ninavaa barakoa, nina nawa mikono yangu kwa sabuni, na ninatumia sanitiza kuzuia maambukizo ya COVID-19.
Anaongeza: “Kwa sababu sijui hali hii itadumu kwa muda gani, nina mpango wa kuimarisha biashara yangu mpya ya kuuza maandazi na vitumbua kwa kupigia simu wateja wangu kila jioni kuwaomba waweke oda yao kesho.”
Rasilimali hii imeandaliwa kwa msaada wa kifedha kutoka kwa serikali ya Canada uliotolewa kupitia Global Affairs Canada.